Tuesday, August 18, 2015

MAUAJI YA KUTISHA WILAYANI KYERWA

Na  Juhudi    Felix-Kyerwa

Watu  watano  wa  familia  moja  katika  Kitongoji  cha  Omukicherenje   kijiji  cha  Mugaba   Kata  ya  Businde  wilayani  Kyerwa  Mkoa  wa  Kagera  wameteketezwa  kwa  moto  na  mashamba  yao  yenye  ukubwa  wa  hekali  15 na   nyumba  nane  zimeteketezwa  na  vitu  vilivyokuwemo  ndani  yake  ambayo  thamani  yake  hajajulikana  baada  ya  kutuhumiwa  kumuua  mfanyabiashara  wa  mazao  mmoja  aliyekuwa  amefuata  mzigo  wa  kahawa  kwenye  familia  hiyo.

Wakizungumza  jana  kwenye   eneo  la  tukio wananchi  wa  kijiji  hicho  na  wengine  kutoka  kwenye  vijiji  jirani  vya  kata  ya  Igurwa  ya  wilayani  Karagwe walisema  kuwa   watu  wasijulikana  walipandwa  na  hasira  baada  ya  kuwepo  kwa  taarifa  za  mfanyabiashara  Jovinary   Morandi  kuwawa   na  kufukiwa  kwenye  shamba  la   Datusi  Paulo  ambaye    alikuwa  wakala  wa  mfanyabiashara  huyo wa  mazao  na  kukutwa  na pikipiki  ya  marehemu  huyo  ndipo  wakamtilia  shaka.

Waliouwawa  na  wananchi  hao  ni   Datusi   Paulo  Miaka (36),Lakius  Paulo(30) ambao  walikuwa  ni  wajukuu  wa  Henerico   John miaka  (70)  ambaye  naye  aliuwawa  kwenye  tukio  hilo  la  kusikitisha  kwa  tuhuma  za  kujihusisha    vitendo  vya  kishirikina  na  huyo ndiye  alikuwa  mkuu  wa  familia.

Wengine  waliouwawa   ni  Launtina  Henericko  (68) ambaye  ni  mke  wa  Henerico  John,   Sabiniani  Henerico (35) na  mtoto  anayedhaniwa  kuteketea  ndani  ya  nyumba  ambapo  vyombo  vya  usalama  walishindwa  kuingia  ndani  ili  kuthibitisha  kama  yupo  huyo  mtoto  hii  ni  kutokana   na  kuwepo  moto  mkali   ndani  ya  nyumba  hiyo.

Waliobahatika  kutoroka  kwenye  mkasa  huo  ni  Adriani  Henerico  na    familia  yake  ambaye  alikuwa  mwalimu katika  shule  ya  msingi  Mugaba  lakini  mali   pamoja  na  nyumba   yake  ziliharibiwa  mashamba  kufyekwa  na  kuchomwa  moto.

Mwingine  aliyesalia  katika  familia  ya  Henerico  John  ni  Froliani  Henerico  miaka( 46) ambaye  aliachwa  na  watu  waliotenda  tukio  hilo  kwa  kile  kilichoelezwa kuwa  alikuwa  ametengwa  na  familia  hiyo kipindi  cha  miaka 10 kutokana  na  kutokubaliana  na  vitendo  walivyokuwa  wanavitenda  ndugu  zake.

Akizungumza   na   mwandishi  wa  habari  hii   katika  eneo  la  tukio   Frolian  Henerico   aliyebahatika  kuachwa  salama  na  mali  zake  alisema  kuwa  wananchi  wa  kijiji  hicho  na  maeneo  jirani  walikuwa  wamechoshwa  na  vitendo  vya  ushirikina  na  ujambazi  walivyokuwa  wanafanya  wanafamilia  hao  na  yeye  kuachwa  walikuwa  wakijua  alivyotengwa  na  ndugu  kwasababu  ya  kutokubaliana  nao.

“Ndugu  mwandishi  wa  habari  nimetengwa  na  familia  yangu  kwa  kipindi  cha  miaka  kumi  nimejaribu  kwenda  kwenye  baraza  la  kata  kusuluhisana  lakini   ilishindikana  na  niliambiwa  tukae  tuyamalize  ndiyo  maana  nilikubali  kutengwa    na  ndugu  zangu”Alisema  Frolian


Mwenyekiti  wa  serikali  ya  kijiji  cha  Mugaba  Justinian Clemence  alisema  kuwa  yeye  alifuatwa  nyumbani  na  wananchi   na  ndugu  za  mfanyabishara  aliyeuwawa  wakiwa   na  mwenyekiti  wa  Kitongoji  cha  Omukicherenje wakitaka  kuanza  msako  wa  kumtafuta  ndugu  yao  baada  ya  kuwa  haonikani  na  aliaga  kuwa  anafuata  mzigo  wake  kwa  Datusi   Paulo  ndipo  aliwakubalia  na  kuenda  nyumbani  kwa  mtuhumiwa  huyo.
Alisema  kuwa  baada  ya  kufika    nyumbani  kwa  mtuhumiwa  wakiwa  kwenye  mahojiano  mafupi  waliona  damu  na  kuanza  kufuatilia  ilikoelekea  ndipo  waliona  sehemu  ikiwa  imechimbuliwa  na  walipofukua  waliona  mwili  wa  mtu  ndipo  hasira  za  wananchi  zilianzia  hapo.

Mkuu  wa  wilaya  ya  Kyerwa  Luten  Edward … akiongea  na  wananchi  katika  eneo  la  tukio    na  kujionea  hali  halisi   na  baadae  kuongea  nao  huku  akiwataka  kutojichukulia  sheria  mkononi  kwani  kufanya  hivyo  vyombo  vya  usalama  vitakosa  taarifa  muhimu  za   kiuchunguzi   na  kuongeza  kuwa  wanapopata  taarifa    za  kiuharifu  na  uvunjifu  wa  amani  watoe  taarifa  kwa    vyombo  vya  dola  ili  viweze  kuchukua  jukumu  lake  la  kufanya  uchunguzi  na  hatimaye  sheria  ichukue  mkondo  wake.


“Ni kweli  tukio  hili  linaweza  kukupandisha  hasira  kwani  kumuua   mtu  na  kumfukia  kwenye  shimo   si  jambo   rahisi  lakini  nyinyi  wananchi msiwe  wepesi  wa kujichukulia  sheria mkononi  ona  sasa  aliyeua  ameuwawa  na  ndugu  zake  wengine  mali  na  zenyewe    mmeteketeza   tulizoea  kusikia  kwa  wenzetu  wakulya,  wamasai  lakini  nyinyi akinamshomile  tunajua  ni wastaarabu  lakini  mmeanza  kutisha  kiasi  hiki?”Alihoji  Luten  Mstaafu  Edward


Mkuu  wa  wilaya  alihaidi  kukaa  pamoja  na  wananchi  wa  kijiji  hicho  kwa  ajili  ya  kuongea  nao  kwa  kina  ili  kutafuta  ufumbuzi  wa  tatizo  ili  amani  na  utulivu  ulirejee  kwenye  eneo  hilo  na  wananchi    waweze  kuendelea  na  shughuli  zao  za  uzalishaji.






Hata  hivyo  hadi  mwandishi  wa  habari  hii  anatoka  kwenye  eneo  la  tukio  aliacha  jeshi  la  polisi  wakiendelea  na  taratibu  za  kiuchunguzi  na  kusema  kuwa  watatoa   taarifa  rasmi   na  mwili  wa  mfanyabiashara  aliyeuwawa  ulifukuliwa na  kufanyiwa  uchunguzi  na daktari  kisha  kuupeleka  kwenye  chumba  cha  kuhifadhia  maiti  kwenye  hospitali  ya  Nyakahanga  wilayani  Karagwe,huku  miili  ya  waliochomwa moto   kukabidhiwa  kwa  uongozi  wa  serikali  ya  kijiji  cha  Mugaba kwa  ajili  ya  taratibu  za  mazishi.


Vitendo  vya   wananchi  kujichukulia  sheria  mkononi    katika  wilaya  ya  Karagwe  na  Kyerwa  kwa  mwezi  wa  saba   vinazidi  kuongezeka  kila  siku  ambapo   Julai  8   mwaka  watu  wanne(4)  waliuwawa  katika  kijiji  cha  Kanogo  kata  ya  Nyakabanga     Julai 14 mwaka  huu  watu wanne(4)waliuwawa  katika  eneo  la  masheshe  kata  ya  Nyakasimbi  wote  waliouwawa  walituhumiwa  kujiuhisha  na  vitendo  vya  uharifu  kwenye  jamii.

No comments:

Post a Comment