MADIWANI
wa halmashauri ya wilaya ya Biharamulo mkoani kagera wameweka kando
tofauti zao za kisiasa na kulazimika kususia kikao cha baraza hilo
kutokana na kumtuhumu mkurugenzi wa halmashauri hiyo Alhaji Zuber Mbyana kupuuza maazimio ya vikao halali vya madiwani.
Hatua
hiyo imetokana na taarifa iliyowasilishwa na diwani wa viti maalumu
Ziyuni Hussen baada ya kutoa hoja ya kulitaka baraza hilo kususia kikao
hicho kwa madai mkurugenzi wa halmashauri hiyo amekuwa akikaidi kutekeleza
mambo mbalimbali wanayoyaadhimia kwenye vikao vya baraza hilo na kwamba
amekuwa akitekeleza mambo anayotaka yeye mwenyewe.
Baadhi ya mambo yaliyopelekea kususia kikao hicho ni pamoja na kutotekelezwa azimio la madiwani hao kwenda kutembelea mgodi wa dhahabu wa TULAWAKA ili kujionea shughuli zinazofanywa na wawekezaji hao na kuwataka kulipa kwa wakati malipo ya mrahaba wa kiasi cha shilingi 300 milioni kwa mwaka.
Mbali
na hilo ni pamoja na kutaka kutembelea kwenye msitu wa hifadhi ya taita
ya Burigi kwa lengo la kujionea uharibifu wa mazingira ambao
umesababishwa na baadhi ya wahamiaji haramu kuweka makazi,mifugo,ukataji
miti ya kupasua mbao,kilimo na uchomaji mkaa kinyume cha sheria.
Kutokana na hali hiyo walidai kushindwa kutekelezwa kwa maazimio hayo kunaonyesha wazi jinsi mkurugenzi wao asivyokuwa makini na utumishi wake na badala yake amekuwa akifanya kazi kwa mazoea hali inayopelekea baadhi ya madiwani kutokuwa na imani naye.
Katika kikao hicho ambacho kilidumu kwa takribani dakika 2 muda mchache baada ya kaimu mkurugenzi wa halmashauri hiyo Zabron
Njanga kusimama kwa lengo la kufungua kikao ambapo ilitolewa taarifa
kutoka kwa diwani Hussen akimtaka mwenyekiti wa kikao hicho kusitisha
baraza hilo kwa madai ya kutokuwa tayari kujadili ajenda mpya
zilizowasilishwa mbele yao kingali maamuzi ya awali yakiwa
hayajatekelezwa.
Hatua
hiyo ilipelekea madiwani hao kuweka kando tofauti zao za kisiasa na
kuungana kwa pamoja kususia baraza hilo huku wakionekana kutetea maamuzi
hayo kwa madai litakuwa fundisho kwa viongozi wengine kutekeleza maamuzi yanayotolewa na vikao halali vya madiwani.
Kaimu mwenyekiti wa halmashauri hiyo Laurent Kakuru
alisema hatua ya madiwani hao ilikuwa sahihi na kwamba anaungana na
hoja za madiwani hao kutokana na maamuzi ya vikao kupuuzwa huku
akiwatupia lawama baadhi ya watumishi wa halmashauri hiyo kujihusisha na
mianya ya rushwa kinyume cha sheria.
“Hata
mimi ninaungana na maamuzi ya madiwani wenzangu kwa kuwa mkurugenzi
wetu amekuwa hatekelezi baadhi ya maamuzi yetu…kwani tuliomba kutembelea
kwenye vivutio vya hifadhi ya taifa ya Burigi lakini hakuna majibu ya
kulidhisha…pia tuliomba kutembelea mgodi wa dhahabu wa Tulawaka lakini
bado suala hilo limekuwa kitendawili” alisema Kakuru
Kwa
upande wake mnadhimu wa kambi ya upinzani ya madiwani wa chadema
wilayani humo Josephat Kayamba ameupongeza uamuzi uliofikiwa na madiwani
hao na kwamba hatua hiyo ni mwanzo mzuri kwa madiwani wa chama tawala
kusimamia maamuzi yanayoamuliwa badala ya kuwa mashabiki wa kupinga hoja
zinazoibuliwa na madiwani wa upinzani.
Alisema
tamko la Chadema ni kuwa linamtaka mkurugenzi wa halmashauri hiyo
kuitisha kikao cha baraza jingine ndani ya siku 21 ili waweze kutoa
taarifa ya tume iliyoundwa kuchunguza ubadhilifu wa fedha za miradi ya
maendeleo.
Aidha
walionyesha kuwa na mashaka ya upatikanaji wa hati safi katika
halmashauri yao na kulazimika kuhoji vigezo vinavyotumika kutokana na
halmashauri hiyo kuwa ya mwisho katika ukusanyaji mapato ya vyanzo vya ndani kwa kipindi cha robo tatu ya mwaka2011/2012 katika mkoa wa kagera.
Akijibu tuhuma hizo kaimu mkurugenzi huyo
alikanusha vikali madai yaliyotolewa na madiwani kwa kuwa ofisi yake
ilikuwa na majibu ya kutosha kuhusiana tuhuma zilizoelekezwa kwenye
ofisi hiyo.
No comments:
Post a Comment