Thursday, May 10, 2012

TAKUKURU KAGERA YALALAMA

NaMbeki Mbeki ,
 
TAASISI ya kuzuia na kupambana na rushwa (TAKUKURU) mkoani kagera imekiri kuelemewa na udhibiti wa kesi za rushwa kutokana na watu wengi kutotoa ushirikiano kwa taasisi hiyo,mkanganyiko wa baadhi ya habari zinazoripotiwa kwenye vyombo vya habari kuharibu mwenendo wa upelelezi,pamoja na vitendo vya rushwa kufanyika kwa siri kubwa.
Akizungumza kwenye mafunzo maalumu ya waandishi wa habari mkoani kagera (KPC) Mwezeshaji wa taasisi hiyo Doreen Kapwani alisema rushwa kamwe haiwezi kwisha katika jamii kwa kuwa ilikuwepo tangu enzi za mababu,huku akitolea mfano wa dhambi kuendelea kutendeka licha ya viongozi wa dini kukemea hali hiyo kila mara.
Kufuatia hali hiyo alisema Taasisi hiyo imelazimika kutoa mafunzo maalumu kwa waandishi wa habari ili kuwajengea uwezo wa kuandika habari za kufichua vitendo vya rushwa hasa vijijini kwa lengo la kudhibiti ubadhilifu wa fedha za miradi ya Umma,taasisi na watu binafsi.
Alisema vyombo vya habari ni nguzo muhimu sana katika kupambana na vitendo vya rushwa katika jamii na kwamba taasisi hiyo imeamua kufufua mahusiano mapya na waandishi wa habari nchini baada ya kuwepo ukimya wa vyombo vya habari kuripoti habari zinazohusu rushwa.
Kwa mujibu wa mkuu wa wilaya ya Bukoba Samwel Kamote ambaye pia alikuwa mgeni rasmi katika uzinduzi wa mafunzo ya siku tatu yaliyoanza jana,viongozi wote wa serikali wanatakiwa kuwa wazi kwa waandishi wa habari katika kueleza mambo ambayo wangependa kupata ufafanuzi badala ya kuficha habari hizo ambazo ni mhimu kwa jamii.
Kamote alisema kushindwa kutoa ushirikiano kwa waandishi wa habari ni kujenga tabaka bovu ambalo linaweza kusababisha uvunjifu wa amani kwa jamii,baada ya kuandikwa habari ambazo hazina usahihi.
Kuna haja kubwa kwa vyombo vya habari nchini kujikita zaidi katika kuandika habari za vitendo vya rushwa kwa kuwa visipo ibuliwa vinaweza kuendelea kuathiri zaidi wananchi maskini,hivyo kupelekea  kukosa imani na serikali yao.
Alidai kuwa waandishi wa habari wanatakiwa kuwa na ushirikiano mkubwa na taasisi ya kuzuia na kupambana na rushwa badala ya kuweka daraja dhidi yao hali ambayo inaweza kusaidia kupunguza vitendo vya kutoa na kupkea rushwa.                                                                               

No comments:

Post a Comment