Wednesday, June 6, 2012

KILA KAZI HUWA NA ADHA YAKE MWANDISHI ASHUSHIWA KIPINGO HUKO BUKOBA

 Na Mwandishi wetu.
Bukoba
MEYA wa Manispaa ya Bukoba Dkt Anatory Amani anadaiwa kumkwida shati na kumfukuza mwandishi  wa habari wa gazeti la Mtanzania ofisini kwake akimtuhumu kuandika habari za kupotosha kuhusu mradi wa ujenzi wa soko jipya la Bukoba.
 
Kwa mujibu wa maelezo yaliyofunguliwa katika kituo cha polisi Bukoba katika faili namba BU/RB/3161/2012 mlalamikaji ambaye ni Mwandishi wa gazeti la Mtanzania Audax Mutiganzi anadai tukio hilo lilitokea juzi alasiri katika ofisi ya kiongozi huyo.
 
Katika maelezo yake Mutiganzi anadai kuwa alifika katika ofisi za Manispaa akiwa na ofisa mkuu mtendaji wa benki ya posta nchini na Sabasaba Moshingo aliyekuwa kwenye ziara ya siku mbili mkoani Kagera.ambao walikwenda kufanya mazungumzo ya kupatiwa kiwanja cha ujenzi wa ofisi ya benki yao.
 
Pia katika maelezo yaliyofunguliwa na  mwandishi huyo anadai baada ya kuingia katika ofisi ya Dkt Anatory Amani,kiongozi huyo ambaye ni Meya wa Manispaa ya Bukoba alimfokea na kumwamuru kuondoka katika ofisi yake haraka iwezekanavyo.
 
Mlalamikaji anadai kuwa Meya huyo alimtuhumu kuandika habari za upotoshaji juu ya mradi wa ujenzi wa soko jipya na kuwa alimkwida shati,kusukuma nje huku akibamiza mlango kwa nguvu.
 
Baadhi ya viongozi waliotajwa katika maelezo hayo kuwa walishuhudia tukio hilo ni Ofisa Mkuu Mtendaji wa Benki ya Posta nchini Sabasaba Moshingo,Meneja wa tawi la Bukoba Maduhu Makoye na Kaimu Mkurugenzi wa Manispaa hiyo Stephene Nimzihirwa ambapo mtuhumiwa alikwenda kutoa taarifa kituo cha polisi.
 
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kagera Henry Salewi alitotafutwa ili kujua hatua zitakazochukuliwa wasaidizi wake walisema hayupo ofisini na hata simu yake ya mkononi iliita bila kujibiwa.
 
Pia mlalamikiwa ambaye ni Meya wa Manispaa Dkt Anatory Aman simu yake iliita muda mrefu bila kujibiwa pamoja na kutumiwa ujumbe mfupi wa maneno kuwa waandishi wa walitaka kujua na kusikia upande wa Meya huyo dhidi ya malalamiko yaliyopo kituo cha polisi ambapo namba ya Meya huyo ni 0767428607.
 
Pia hivi karibuni kupitia barua kumbukumbu namba BMC/120/16/30 ya May 17,2012 iliyosainiwa na Mkurugenzi wa Manispaa hiyo Hamis Kaputa na kusambazwa kwenye vyombo vya habari mjini hapa  iliwaonya waandishi kuwa wanapotosha taarifa za maamuzi halali ya vikao.
 
Pia barua hiyo inawatahadharisha waandishi juu ya kurudiwa mara nyingi kwa habari zilizodaiwa zimepotoshwa na kuwa Manispaa iko tayari kuchukua hatua za kisheria kama upotoshaji huo ungeendelea.
 
"Wasemaji wa Manispaa ni Mstahiki Meya na Mkurugenzi au atakayekasimiwa madaraka na sio vinginevyo,ofisi yetu ipo tayari wakati wowote kuwapa waandishi habari sahihi"inasema sehemu ya barua hiyo.
 
Manispaa ya Bukoba ipo mbioni kutekeleza miradi ya ujenzi wa soko jipya,kituo kipya cha mabasi na upimaji na uuzaji wa viwanja 5,000 miradi inayotafsriwa kuwa haiwezi kutekelezwa kwa ufanisi  kwa wakati mmoja na badala yake itakuwa mzigo kwa Manispaa na wananachi.

No comments:

Post a Comment